![]() |
| Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu |
Na Mwandishi wetu
MBUNGE wa Singida Mashariki kupitia chama cha Democrasia na
Maendeleo (Chadema), Tundu Lissu, amekamatwa na Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya
Dar es Salaam leo dakika chache baada ya kufutiwa mashtaka ya uchochezi
yaliyokuwa yakimkabili.
Lissu
amekamatwa akiwa ndani ya Mahakama ya Kisutu ambayo leo ilitoa uamuzi wa kufuta
kesi ya uchochezi iliyokuwa ikimkabili baada ya serikali kuwasilisha taarifa
kuwa haina nia ya kuendelea na kesi hiyo.
“Nimekamatiwa Mahakamani Kisutu. Sikutoka hata nje ya mahakama
nikakamatwa tena. Wamenipeleka Central kwa mahojiano, polisi walionikamata
wamekataa kuniambia wananikamata kwa kosa gani,” amesema Lissu katika taarifa
aliyoandika na kusambaza akiwa mikononi mwa polisi.
Lissu amedai kuwa, anaamini kukamatwa kwake kuna uhusiano wa
moja kwa moja uchaguzi ujao wa Chama cha Mawakili hapa nchini (TLS),
unaotarajia kufanyika wiki mbili zijazo.
“Serikali hii, kwa kutumia mawakili wao vibaraka, imekuwa na
mkakati mkubwa wa kunizuia kugombea urais wa TLS. Walipanga kwenda kupinga
kugombea kwangu mahakamani. Tumewasema hadharani na kuzianika njama zao. Sasa
wameamua kutumia rungu lao la siku zote.
“Hofu yao ni kubwa sana. Natabiri watataka kuniweka ndani hadi
baada ya uchaguzi huo. Mawakili vibaraka wao wataleta hoja kwenye TLS kwamba
mgombea asiyekuwapo ukumbini wakati wa Uchaguzi aondolewe kwenye kinyang’anyiro
hicho,” ameandika.
Lissu ameeleza kuwa hakuna makatazo yoyote katika kanuni za
uchaguzi yanayozuia mgombea kuondolewa kwenye uchaguzi kwasababu tu hayupo
ukumbini na amewataka mawakili washikilie msimamo kwamba wote walioteuliwa
kugombea wapigiwe kura.
“Nimekamatwa asubuhi na mapema. Hakuna sababu ya kutokunipeleka
mahakamani leo. Kama hawatanipeleka mahakamani, nitaanza mgomo wa kula chakula,
sitakula hadi nitakapopelekwa mahakamani,” amesema.


0 Michango:
Post a Comment